Thursday, October 21, 2010

Karatasi za kura zabadilishwa

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imetangaza mabadiliko katika karatasi ya kupigia kura .

Wananchi watakaopiga kura watapaswa kuweka alama ya vema kulia kwa mgombea wa chama anachokusudia kukichagua badala ya chini ya picha ya mgombea.

Pia Tume imesema zaidi ya Watanzania milioni 19.6 waliojiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura wanatarajia kupiga kura Oktoba 31, Tanzania Bara kuchagua Rais, wabunge na madiwani.

Ofisa wa Tume hiyo, Anna Ruganyoisa, alisema hayo jana wakati akizungumza na viongozi wa vyama vya siasa ngazi ya mkoa.

Alisema, wagombea 8,980 wameteuliwa na Tume na wanatarajiwa kupigiwa kura; wagombea urais wakiwa saba, ubunge 1,041 na udiwani 7,932.

Alisema kabla ya kupiga kura vifaa vitakabidhiwa kwa wasimamizi wa vituo mbele ya mawakala na kutolewa idadi yao ikiwa ni pamoja na karatasi za kupigia kura kwa kufuata Daftari.

Akifungua mkutano huo, Makamu Mwenyekiti wa NEC, Jaji Omari Makungu, alisema kuwa kuanzia Oktoba 12, karatasi za kupigia kura zilishaanza kusafirishwa kwenda majimboni na vifaa vingine ikiwa ni pamoja na kuanza upangaji wa vifaa kwa kila kituo.

Alisema, katika hatua ya mwisho, vyama vinapaswa kuzingatia kuchagua wakala mmoja kwa kila kituo, na kuhimiza wapangwe kwenye kata zao, ili kutambua wapiga kura nao waweze kupiga kura.

Jaji Makungu alisisitiza kuwa, mawakala wana wajibu mkubwa kwa vyama vyao ikiwa ni pamoja na kuhakikisha anayepiga kura ndiye aliye kwenye Daftari, pili, kuhakikisha sheria na kanuni za uchaguzi zinafuatwa na mwisho, ni kulinda maslahi ya chama, hivyo kuviomba vyama kuteua mawakala wanaowaamini.

Tume ilitoa angalizo kwa wapiga kura na viongozi wa vyama, kuwa katika karatasi za kupigia kura, kutakuwa na mabadiliko hivyo wasome na kuzielewa vizuri na kuweka alama.

Oscar Job anaripoti kwamba, Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IJP) Said Mwema, amekanusha taarifa za kuingizwa kwa karatasi za kura nchini zinazodaiwa kuwekwa alama ya vema kwa mmoja wa wagombea urais.

Mwema alitoa kauli hiyo jana katika hafla ya utiaji saini mkataba wa ushirikiano wa masuala ya teknolojia ya mawasiliano (Teknohama) baina ya Polisi na Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT), uliolenga kuimarisha na kuboresha utendaji wa shughuli mbalimbali za Jeshi hilo.

Alisema katika hali ambayo si ya kawaida, kuna watu walisambaza taarifa za uongo juu ya kuingizwa kwa karatasi za kupigia kura, na kwamba Jeshi hilo baada ya kufanya uchunguzi wake, kwa kushirikisha baadhi ya waliotoa taarifa hizo, lilibaini kutokuwapo ukweli wowote juu ya suala hilo.

“Bila shaka kila mmoja anatambua suala la uchaguzi lililopo mbele yetu kwa sasa, hivyo katika maandalizi ya uchaguzi huo, taarifa mbalimbali zimeanza kusambazwa likiwamo hili la kuingizwa karatasi za kura, jambo ambalo si la kweli,” alisema Mwema.

Awali wakitiliana saini makubaliano hayo, Mwema na Mkuu wa DIT, Profesa John Kondoro walisema pamoja na mambo mengine, mkataba huo utaisaidia Polisi kutoa huduma za kitaalamu katika jamii, likiwamo suala la usalama barabarani.

Imeandikwa na Grace Chilongola, Mwanza; Tarehe: 20th October 2010(habari leo)

No comments: