Tuesday, June 10, 2014

Mgomo wa Daladala Mbeya

Mbeya, leo kumekuwa na mgomo wa daladala za kutoka Uyole kuelekea Sokomatola. Mgomo wenyewe umetokana na sababu za kijinga kijinga tu ukizisikia. Kwamba kwakuwa wameambiwa wabadili njia pale maeneo ya Soweto ili kuepusha msongamano hasa nyakati za asubuhi na jioni basi wapewe idhini ya kupandisha nauli ifike shs 500.

Nasema ni ujinga kwasababu, mara kadhaa nimepanda daladala na zikapita maeneo hayo na nikawasikia madereva na makonda wakisema kuwa inawapa mwanya wa kupata abiria hususan nyakati za mchana na jioni kwani kuna wanaoenda kuwaona wagonjwa, na pia kupata abiria wa sokoni pale Soweto kwa wingi. Kwahiyo kwa upande mmoja mabadiliko hayo yamewanufaisha sana tu.

Lakini pia, mabadiliko haya hayajaongeza urefu wa safari kwa kiwango cha kuwafanya wadai kuwa wanapata hasara. Kwa wanaokaa Mbeya watakuwa wanaelewa hili. Sasa haya madai ya waongeze nauli yanaletwa na nini hasa?

Na ikumbukwe kuwa hata viwango vya sasa vya nauli walipandisha kwa mgomo wakati mafuta yamepanda bei kwa shilingi zisizofikia 100. Lakini yaliposhuka hawakushusha viwango hivyo vya nauli. Na iliwahi hojiwa, inakuwajr mafuta yakipanda wanadai kipandisha nauli tena wanaongea huku mapovu yakiwatoka midomoni lakini yanaposhuka hawashushi?

Kiukweli kabisa, ili kudhibiti hali hii, ningemuomba Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, kwa kushirikiana na SUMATRA, wafute leseni za wote waliogoma na kutangaza kutoa upya leseni kwa ruti hiyo na zingine zitakazoleta shida, kwa wale ambao watakuwa tayari kufuata taratibu ambazo zinakuwa na manufaa kwa watoa huduma na wahudumiwa pia. Tukiendekeza kukinga mikono kwa hawa mabwana kila wanapokohoa na kuwaambia wateme tu mate yao tutakinga kwakuwa tunawapenda na kuwathamini sana, iko siku watazusha makubwa zaidi na vilio kwetu vitakuwa vikubwa zaidi.

Hatuwezi kuishi humu nchini kama tuko kwenye bwawa la kambale. Kila mmoja ana sharubu kwahiyo anajiona mkubwa na anaweza amua anachotaka yeye. Ujinga mtupu.

Rama Msangi,
Kalobe, Mbeya

No comments: